Watu 14 wafariki dunia katika kimbunga Alabama

Muktasari:

  • Gavana wa eneo hilo ametoa tangazo kwa wananchi hao kwamba huenda hali ikabadilika na kuwa mbaya zaidi hapo baadaye

Alabama, Marekani. Zaidi ya watu 20 wamepoteza maisha baada ya kimbunga kupiga katika kaunti ya Lee, Alabama nchini Marekani.

Kwa mujibu wa mkuu wa polisi wa eneo hilo, Jay Jones kikosi cha uokoaji kinatarajiwa kufanya kazi usiku kuondoa miili ya waliofariki na majeruhi kutoka kwenye vifusi vya mamia ya nyumba.

Kamanda Jones amesema tatizo ni kiwango kikubwa cha vifusi vilivyoko katika maeneo yaliyokuwa na nyumba hizo na kwamba huenda idadi ya vifo ikaongezeka.

Hali mbaya ya hewa ndiyo iliyosababisha kimbunga hicho kilichovamia eneo la Kusini mwa Marekani mchana wa jana.

Kulikuwa na taarifa za kuonya kuhusu kimbunga katika maeneo ya Georgia na Alabama kutwa nzima.

Gavana wa Alabama Kay Ivey amewaonya wananchi wa eneo hilo kwamba kunatazamiwa hali mbaya zaidi ya hewa.