Watu 49 wauawa msikitini New Zealand

Muktasari:

Shambulizi linaloshukiwa kuwa la kigaidi limetokea katika misikiti miwili nchini New Zealand na kusababisha vifo na majeruhi

Wellington, New Zealand. Watu 49 wameuawa na wengine zaidi ya 20 wamejeruhiwa baada ya kuzuka mashambulio katika misikiti miwili katika mji wa Christchurch nchini New Zealand.

Kamishna wa polisi, Mike Bush amesema wanaume watatu na mwanamke mmoja wamekamatwa wakihusishwa na tukio hilo huku akisisitiza kuwa huenda washukiwa wengine zaidi wakakamatwa.

Duru za habari zinasema washambuliaji hao hawakuwa kwenye orodha ya magaidi wanaosakwa lakini ni wazi kwamba wana itikadi kali.

Waziri Mkuu wa Australia, Scott Morrison amesema mojawapo ya waliokamatwa ni raia wa Australia. Amemtaja mshukiwa wa shambulio hilo kuwa "gaidi mwenye itikadi kali za mrengo wa kulia".

Baadhi ya watu walioshuhudia tukio hilo wameviambia vyombo vya habari kuwa walilazimika kutoroka kuokoa maisha yao na waliona watu walioanguka chini wanaovuja damu nje ya msikiti wa Al Noor.

Polisi inasisitiza kwamba hali bado haijaimarika na wamethibitisha pia kwamba "vilipuzi kadhaa vilivyofungwa kwenye gari vimeharibiwa".

Mwanamume wa Palestina ambaye alikuwa katika moja ya misikiti hiyo alisema aliona mtu akipigwa risasi kichwani.