DC ashinda kura za maoni kumrithi Lissu

Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Miraji Mtaturu

Singida. Mkuu wa Wilaya ya Ikungi, Miraji Mtaturu amepitishwa na mkutano mkuu wa CCM wa Wilaya hiyo kuwania ubunge wa Singida Mashariki.

Mtaturu ametangazwa jana jioni msimamizi wa uchaguzi huo uliofanyika wilayani humo, Salum Reja ambaye ni katibu wa sekretarieti ya Taifa ya chama hicho.

Reja alisema Mtaturu alipata kura 396 akifuatiwa na Mugoto Kitima aliyepata kura 79 huku mkuu wa Mkoa wa zamani wa Songwe, Chiku Galawa akipata kura 40.

“Kura zilizopigwa zilikuwa 600 na hakuna kura iliyoharibika,” alisema Reja.

Baada ya kutangazwa mshindi, Mtaturu aliwashukuru wajumbe hao na kuahidi kushirikiana na wananchi na viongozi katika kuliletea maendeleo jimbo hilo.

Uchaguzi huo utafanyika Julai 31 baada ya Spika wa Bunge, Job Ndugai kutangaza kuwa aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Tundu Lissu amepoteza sifa za kuwa mwakilishi wa wananchi kwa kushindwa kutoa taarifa za mahali alipo pamoja na kutojaza fomu za mali na madeni.

Kutokana na hatua hiyo, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Julai 5, ilitangaza ratiba ya uchaguzi huo.