Taxify yabadili jina, sasa kuitwa Bolt

Muktasari:

  • Taxify ambayo ni kampuni inayotoa huduma za usafiri, imebadili jina lake ili kwenda sambamba na malengo yake kibiashara

Dar es Salaam. Kampuni inayotoa huduma za usafirishaji barani Afrika na Ulaya ya Taxify imebadilisha nembo na jina lake na kuanza kuitwa Bolt.

Mabadiliko hayo ya alama ya utambulisho wa kampuni yamelenga kwenda sambamba na malengo ya kampuni katika huduma zake za usafiri.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Alhamisi Machi 7, 2019 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji na mwanzilishi mwenza wa Bolt, Markus Villig amesema jina hilo la Bolt litaanza kufahamika hatua kwa hatua katika masoko ya kimataifa katika wiki zijazo.

Alisema Taxify ilizinduliwa miaka mitano iliyopita kwa malengo ya kutoa huduma za usafiri mijini kwa njia rahisi na bei nafuu.

Naye Meneja Mkazi wa Bolt nchini Tanzania, Remmy Aseka alisema bidhaa ya kwanza ya kampuni hiyo ya usafirishaji ilikuwa ni kutoa suluhisho na kurahisisha upatikanaji wa huduma za teksi kwa wateja wake.