Baba wa Alikiba afariki baaada ya kulazwa Muhimbili kwa siku 21

Muktasari:

Baba wa msanii Alikiba amefariki dunia leo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili alipokuwa akipatiwa matibabu tangu Desemba 27 mwaka jana.

Baba wa msanii AliKiba, Saleh Kiba amefariki dunia leo katika hospitali ya Muhimbili alipokuwa amelazwa kwa takribani siku 21 .

Akizungumza na Mwananchi mdogo wa Alikiba,  Abdu Kiba, amethibitisha kutokea kwa kifo hicho.

Hata hivyo, alipotakiwa kueleza kwa undani chanzo cha kifo cha baba yao, Abdu ambaye pia ni mwanamuziki anayefanya kazi chini ya usimamizi wa kaka yake alisema hayupo katika mazingira mazuri ya kulizungumzia hilo  na kutaka mwandishi amtafute baadaye.

Kuhusu msiba ulipo, alisema upo maeneo ya Kariakoo Mtaa wa Muheza ambapo ndipo nyumbani kwao.

Naye Ofisa Uhusiano wa hospitali ya Taifa ya Muhimbili(MNH), Neema Mwangomo, amesema Mzee Saleh, alifikwa na mauti leo saa 12:05 katika hospitali hiyo.

Neema alibainisha kwamba baba huyo alifikishwa hospitalini hapo tangu Desemba 27 mwaka jana.