Boko haram tishio uchaguzi Nigeria
Muktasari:
Zaidi ya Wanigeria milioni 84 wameandikishwa kupiga kura kwenye taifa hilo lenye wakaazi milioni 190 la Magharibi mwa Afrika
Lagos,Nigeria.Wakati leo wananchi wa Nigeria wakijitokeza vituo vya kupigia kura kwenye Uchaguzi ulioahirishwa kwa wiki moja baadhi ya watu wanahofia kushambuliwa na kundi la Boko Haram.
Hata hivyo Rais Muhammadu Buhari amewataka wananchi wa wajitokeze kwenda kupiga kura leo Jumamosi na ameahidi kwamba utakuwepo usalama wa kutosha.
Katika uchaguzi huo ulioahirishwa wiki iliyopita Rais Buhari atachuana vikali na mfanyabiashara Atiku Abubakar ambaye hapo awali alikuwa makamu wa rais.
Tume huru ya uchaguzi wiki iliyopita iliahirisha uchaguzi huo wakati Wanigeria zaidi ya milioni 72 walipokuwa wanajitayarisha kwenda kupiga kura.
Akilihutubia taifa kwenye televisheni Rais Buhari amewataka Wanigeria wasiwe na wasiwasi na wawe na imani kuhusu usalama na pia Tume ya Uchaguzi itatimiza jukumu lake.
Naye mpinzani wa Buhari ambaye ni kiongozi wa chama kikuu cha upinzani PDP Atiku Abubakar ametoa wito huo huo kwa wapiga kura.
Lakini kwenye maeneo mengi ya Kaskazini, ambako uasi wa kundi la Boko Haram umesababisha vifo vya zaidi ya watu 27,000 na kuwafanya mamilioni kuyakimbia makazi yao. Maelfu ya watu huenda wasiweze kushiriki kwenye uchaguzi huo.
Wananchi waishio Kaskazini walilazimika kuyakimbia makaazi yao kutokana na kushambuliwa mara kwa mara na kundi la kigaidi la Boko Haram.
Hali ambayo imepoteza hamu ya kupiga kura ingawa wanatarajia matokeo ya kura hiyo yatarudisha tena amani kwenye maeneo yaliyotawaliwa na matumizi ya nguvu.