Mwanamke achaguliwa Spika DRC

Jeanine Mabunda

Muktasari:

Ni mwanamke wa kwanza kuwa Spika nchini Jamhuri ya Congo

Kinshasa, DRC. Wabunge wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, wamemchagua Jeanine Mabunda kutoka muungano wa FCC kuwa Spika mpya wa Bunge.

Mabunde alikuwa mgombea pekee baada ya mpinzani wake, Henri Thomas Lokondo, kuondolewa na zoezi hilo kususiwa na wabunge wa upinzani wakisema halikuwa huru na haki.

Spika mpya anatokea muungano wa siasa unaomuunga mkono rais wa zamani, Joseph Kabila na anakuwa mwanamke wa kwanza kuchaguliwa kushika nafasi hiyo.

Hata hivyo, Lokondo aliyeondolewa katika uchaguzi huo amesema alikuwa na uhakika wa kushinda.

Wakati huohuo, vyama vya upinzani vinavyojumuika kwenye muungano wa Cash wa Rais, Felix Tshisekedi, wamejitoa kwenye kamati kuu ya Bunge wakisema  wamenyimwa nafasi zao walizoahidiwa kwenye Bunge.

Hata hivyo, wabunge hao wamesema wataendelea kushiriki vikao vya Bunge kwa kutekeleza majukumu waliopewa na wananchi.