Hawa ndio mabalozi wa utalii Tanzania, Mbwana Samatta, Diamond na Ali Kiba ndani

Muktasari:

Wizara ya Maliasili na Utalii leo Ijumaa Mei 24, 2019 imetaja baadhi ya majina ya mabalozi wa Utalii nchini, akiwemo Mbwana Samatta, Mtanzania anayecheza soka ya kulipwa nchini Ubelgiji katika klabu ya KRC Genk

Dodoma. Wizara ya Maliasili na Utalii leo Ijumaa Mei 24, 2019 imetaja baadhi ya majina ya mabalozi wa Utalii nchini, akiwemo Mbwana Samatta, Mtanzania anayecheza soka ya kulipwa nchini Ubelgiji katika klabu ya KRC Genk.

Akizungumza leo Ijumaa Mei 24, 2019 jijini Dodoma, Dk Kigwangalla amesema tayari Samatta ambaye ni nahodha wa Taifa Stars ameanza kuonyesha mafanikio makubwa kwa kuitaja Tanzania kila mahali.

Mabalozi wengine wa utalii ni wasanii Ali Kiba na Diamond Platnumz  na  wanamitindo, Flaviana Matata na Miriam Odemba.

Kuhusu Samatta, Dk Kigwangala amesema walimtaka mchezaji huyo awe anataja zaidi jina la Tanzania, kuzungumza lugha ya Kiswahili mara nyingi, kuipeperusha bendera ya Taifa mara kadhaa na wako mbioni kumalizia mazungumzo ili kuialika timu ya Genk kuja nchini.