Hatimaye Barcelona yamnasa Grizmann, yamwekea bei mbaya kutoa Catalunya

Antoine Griezmann

Muktasari:

  • Griezmann alikuwa mmoja wa wachezaji walioiongoza Ufaransa kutwaa Kombe la Dunia mwaka jana wakati fainali hizo zilipofanyika Russia.

Madrid, Hispania . Barcelona imetangaza kumsajili Antoine Griezmann leo Ijumaa kwa ada ya dola 135 milioni, na kuamsha manbeno kutoka Atletico Madrid kuhusu kiwango ambacho mabingwa hao wa soka wa Hispania wamelipa kumnasa nyota huyo aliyetwaa Kombe la Dunia na Ufaransa.
Katika taarifa yake, Barca iliweka bayana kuwa imelipa euro 120 milioni kuwezesha kukabiliana na kipengele cha kumuwezesha mchezaji huyo kuruhusiwa kuondoka, ikiongeza kuwa atasaini mkataba wa miaka mitano ambao utajumuisha kipengele kama hicho (buyout clause) lakini kilichowekewa kiwango cha juu zaidi cha fedha, euro 800 milioni.
Hata hivyo, ndani ya dakika chache, Atletico ilisema inaamini kuwa "kiwango cha fedha kilicholipwa hakitoshi matakwa ya kifungu cha kumruhusu (release clause) kwa kuwa ni dhahiri kuwa makubaliano ya mchezaji huyo na Barcelona yalifikiwa kabla ya kifungu hicho kushushwa kutoka euro 200 milioni hadi europ 120" mwanzoni mwa mwezi.
Klabu hiyo ilisema Griezmann alikwenda ofisi za makao makuu ya Shirikisho la Soka la Hispania ((LFP) kuvunja mkataba bila ya upande wa pili kuhusishwa baada ya Barca kuafiki kifungu cha kumruhusu, na kuongeza kuwa "walishaanza taratibu sahihi" za kutetea haki yao na maslahi ya haki".
Taarifa hiyo ni mpya katika mzozo baina ya klabu hizo mbili na Griezmann, ambaye ana miaka 28, hakutokea kwenye kambi ya Atletico Madrid kujiandaa kwa msimu ujao wakati wenzake walipokutana Jumapili baada ya kutangaza mwezi Mei kuwa ataondoka klabu hiyo bila ya kusema anakwenda wapi -- licha ya kwamba kwa muda mrefu amekuwa akiaminika kuwa angejiunga na Barcelona.
Wiki iliyopita, Atletico iliituhumu Barcelona na Griezmann kwa "kukosa heshima" baada ya rais wa Barca, Josep Maria Bartomeu kuweka bayana kuwa klabu hizo mbili zilifanya mazungumzo kuhusu mshambuliaji huyo wa zamani wa Real Sociedad.