Al Bashir siondoki ng’o

Rais wa Sudan, Omar al Bashir

Muktasari:

  • Hivi karibuni Serikali ya Sudan ilisema watu 19 waliuawa wakiwemo wafanyakazi wawili wa usalama tangu maandamano yalipoanza Kaskazini-Mashariki ya mji wa Atbara, Desemba 19 mwaka jana

Khartoum, Sudan. Rais wa Sudan, Omar al Bashir, amesema hataondoka madarakani licha ya shinikizo kutoka kwa waandamanaji wanaotaka aondoke, baada ya miaka 30 ya kuwa katika uongozi wa nchi hiyo.

Waandamanaji nchini Sudan wanataka Al Bashir aondoke madarakani kwa sababu uchumi wa nchi hiyo umeporomoka.

Waandamanaji waliripotiwa kulenga na kuzichoma ofisi za chama cha Al Bashir na walitoa wito wa kumalizika utawala wake wa miaka 29.

Bashir aliingia madarakani katika mapinduzi ya kijeshi mwaka 1989.

Jana polisi walipambana na waandamanaji kwa kurusha mabomu ya machozi katika mji mkuu wa Sudan wakati wa maandamano yanayotoa wito kwa Rais Al Bashir kujiuzulu yakiendelea kwa wiki ya tatu.

Wakati huohuo kundi la kutetea haki za binadamu la Amnesty International lilisema watu 37 wameuawa katika ghasia hizo.

Kutokana na ghasia hizo Serikali ilitangaza kufunga shule na kutangaza amri ya kutotoka nje na hali ya dharura nchini humo katika maeneo kadhaa tangu ghasia zilipoanza.