Alichokisema Joshua Nassari baada ya kuvuliwa ubunge

Muktasari:

Leo Alhamisi, Machi 14, 2019 Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai ametangaza jimbo la Arumeru Mashariki kuwa wazi baada ya mbunge wake, Joshua Nassari (Chadema) kupoteza sifa ya kuwa mbunge

Dar es Salaam. Aliyekuwa mbunge wa Arumeru Mashariki (Chadema), Joshua Nassari amesema ni kweli hakuhudhuria vikao vya mikutano mitatu ya Bunge la Tanzania kama ilivyoelezwa na Spika wa Bunge, Job Ndugai , “lakini nilitoa taarifa.”

Nassari ametoa kauli hiyo baada ya muda mfupi kupita tangu Spika Ndugai kumwandikia barua Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (NEC,) Jaji Semistocles Kaijage kumtaarifu kuhusu jimbo hilo la Arumeru Mashariki kuwa wazi baada ya mbunge wake kupoteza sifa.

Nassari amesema Januari 29, 2019 alimwandikia barua akimtaarifu kwamba asingeweza kuhudhuria mkutano wa 14 wa Bunge kutokana na kuwa nje ya nchi akimuuguza mke wake aliyekuwa amejifungua.

Mbunge huyo amevulia ubunge akiwa anatekeleza majukumu ya kibunge kwasababu alikuwa katika ziara ya kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii iliyokuwa Chuo cha Mweka, Moshi mkoani Kilimanjaro.

“Huu mkutano uliopita (wa Januari 29 hadi Februari 9) nilikuwa nje ya nchi namuuguza mke wangu alikuwa na matatizo ya uzazi na nilimjulisha Spika kupitia barua niliyoituma kwa email (barua pepe),” alisema Nassari

Alisema alifanya hivyo baada ya kuwasiliana na msaidizi wa Spika Ndugai na kumshauri kuandika barua naye akafanya hivyo lakini anashangaa kwa nini amechukuliwa hatua.

Undani zaidi ya alichokisema Nassari na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) usikose gazeti la Mwananchi la kesho Ijumaa Machi 15, 2019