VIDEO: Alichokisema Masele baada ya kuhojiwa

Muktasari:

Leo Jumatatu, Mbunge wa Shinyanga Mjini (CCM), Stephen Masele ambaye pia ni makamu wa kwanza wa Rais wa Bunge la Afrika (PAP) amefika mbele ya kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kujibu tuhuma za utovu wa nidhamu zinazomkabili

Dodoma. Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge imemhoji mbunge wa Shinyanga Mjini (CCM), Stephen Masele kuhusu tuhuma zinazomkabili za utovu wa nidhamu.

Masele amehojiwa na kamati hiyo inayoongozwa na  Emmanuel Mwakasaka leo Jumatatu Mei 20, 2019.

Mbunge huyo ameibua sintofahamu baada ya kutuhumiwa kugonganisha mihimili ya nchi na kwa kile ambacho Spika Job Ndugai alikiita kufanya mambo ya hovyohovyo, hivyo kuitwa arejee nyumbani kutoka Afrika Kusini alikokuwa anahudhuria vikao vya Bunge la Afrika (PAP).

Ndugai aliagiza leo kabla ya saa 5 asubuhi Masele awe ameshafika mbele ya kamati hiyo na Bunge, akisisitiza kuwa pia atahojiwa na kamati ya maadili ya CCM.

Mara baada ya kutoka katika mahojiano Masele amezungumza na wanahabari, “Mimi ninaheshimu  sana viongozi wangu, nimelelewa vizuri na wazazi, nimelelewa vizuri na chama changu, nimetokea umoja wa vijana kuanzia ngazi ya chini kabisa mpaka ngazi ya kitaifa na kuwa mjumbe wa baraza kuu Taifa, nimekuwa mbunge hii awamu ya pili.”

“Nimekuwa naibu waziri katika  natambua miiko ya uongozi, sijawahi kukurupuka, fuatilia rekodi zangu chochote ninachokisema ninasimamia haki, ukweli na ninaheshimu viongozi wenzangu.”

Ameongeza, “Ni matarajio yangu haki itatendeka na mimi sijafanya jambo lolote kinyume na taratibu, kwenye kazi zangu ndani ya Bunge na pia Bunge la Afrika kama makamu wa rais.”

Kuhusu utovu wa nidhamu amesema, “Nawahakikishia Watanzania, nilichokuwa nasimamia ni misingi ya haki za binadamu na kufanya hivyo nisitafsiriwe kwamba ni utovu wa nidhamu.”

Kwa upande wake Mwakasaka amesema baada ya kumhoji Masela watafanya uchambuzi wa mahojiano hayo na watawasilisha taarifa kwa Ndugai.

“Tumemaliza kumhoji na kilichobaki ni uchambuzi wa taarifa,” amesema Mwakasaka bila kubainisha utovu gani wa nidhamu unaomkabili Masele.