Aliwa na Mamba akivua samaki

Muktasari:

  • Mkazi wa kijiji cha Borenga Wilaya ya Serengeti Mkoani Mara ameliwa na mamba wakati akivua samaki katika Mto Mara, Jeshi la polisi mkoani humo limesema familia imeruhusiwa kuchukua mabaki ya mwili kwa ajili ya maziko na msako wa kumtafuta mamba huyo unaendelea.

Serengeti. Maro Mwikwabe (35)mkazi wa kijiji cha Borenga Wilaya ya Serengeti Mkoani Mara ameliwa na mamba wakati akivua samaki katika Mto Mara.

Kamanda wa polisi mkoa wa Mara Juma Ndaki akiongea na Mwananchi Digital leo Jumapili Mei 26 kwa njia ya simu amesema aliliwa na mamba jana (Mei 25,2019).

Amesema mabaki ya mwili wake yalipatikana Mei 25 ndani ya mto Mara na kuhifadhiwa katika hospitali Teule ya Nyerere wilaya ya Serengeti.

"Tumeruhusu ndugu wachukue mwili kwa ajili ya mazishi na taratibu nyingine za kumsaka mamba huyo zinaendelea," amesema.

Mkuu wa Wilaya Nurdin Babu amesema ameagiza askari wa idara ya wanyamapori wilaya kumsaka mamba waweze kumuua.

"Askari toka asubuhi wako eneo la tukio wanaendelea na msako ili waweze kumuua, pia naomba wananchi wachukue tahadhari kuingia mtoni humo kwa kuwa wameishajua kuna mamba," amesema.