Amjeruhi jirani yake kwa shoka akimtuhumu kuiba kuku

Muktasari:

  • Mkazi wa kijiji cha Imalauduki,tarafa ya Ilolangulu, wilayani Uyui, Ramadhani Omary amejeruhiwa kichwani kwa shoka, akidaiwa kuiba kuku wa jirani yake

Tabora. Mkazi wa kijiji cha Imalauduki,tarafa ya Ilolangulu, wilayani Uyui, Ramadhani Omary, amejeruhiwa kichwani kwa shoka, akidaiwa kuiba kuku wa jirani yake.

Tukio hilo limetokea jana saa 2:00 usiku katika kijiji hicho.

Kamanda wa polisi mkoa wa Tabora, Emmanuel Nley amesema leo kuwa, Juma Ndaki anadaiwa kumjeruhi jirani yake kwa kumkata shoka kichwani pamoja na kumvunja mguu wa kushoto.

Ameeleza chanzo cha tukio hilo kuwa ni Juma kumtuhumu Ramadhani kumuibia kuku wake na kuamua kumchukulia hatua kwa kumjeruhi.

Kamanda Nley amesema upelelezi wa tukio hilo unaendelea na mtuhumiwa anashikiliwa na polisi katika kituo cha Ilolangulu na majeruhi anaendelea na matibabu katika hospitali ya rufaa ya mkoa Tabora, Kitete.

 

Mmoja wa wauguzi katika wodi ya majeruhi ya hospitali hiyo aliyeomba hifadhi ya jina lake kwa vile sio msemaji, amesema majeruhi huyo anaendelea vizuri na matibabu na hali yake inazidi kuimarika.