VIDEO: Baba Diamond ajiandaa kushirikiana na Hamisa Mobetto

Muktasari:

Baba wa msanii Diamond Platnumz, Abdul Juma amesema mapokezi aliyoyapata kwenye wimbo ulioachiwa juzi ni wazi kwamba sasa yupo tayari kuimba na Diamond, Queen Darleen na Hamisa Mobeto.

Dar es Salaam. Abdu Juma, ambaye ni baba mzazi wa Diamond Platnumz amesema anashukuru kwa namna wimbo wa Mwewe alioimba kwa kushirikishwa na kueleza sasa yupo tayari kuimba na Diamond, Queen Darleen na Hamisa.

Akizungumza na Mwananchi Digital jana Jumatano Aprili 3, 2019 baba huyo wa watoto wanne, Abdul amesema kundi hilo la wasanii linalojiita Sungura, lilimfuata mara kadhaa kutaka ashirikiane nalo kwenye wimbo.

Anasema hakuona sababu ya kuwakatalia hivyo aliamua kuingia studio na kutoa kibao hicho ambacho ameshirikishwa kwenye kiitikio.

Hata hivyo, Abdul amesema atakuwa mchoyo wa fadhila kama hatawashukuru watoto wake, Queen Darleen na Diamond kwa kuwa kama siyo wao hakuna ambaye angemfuata. 

"Hata nyie waandishi wa habari mmekuwa mkinifuata kwa kuwa watoto wangu ni mastaa, kama sivyo leo angenijua nani mpaka kuna kushangaza watu kwa kuimba jambo ambalo kwangu nililichukulia rahisi kumbe ndivyo sivyo," amesema.

Baada ya kupokewa, amesema anaona ana kila vigezo sasa vya kufanya kolabo na watoto wake na mkwewe, Hamisa Mobeto. 

Baba Diamond amesema yuko tayari wampe mistari tu yeye atatiririka kwani hata wimbo alioufanya ilimchukua dakika kadhaa kuingiza mashairi.