Babu Tale, Harmonize washiriki kumuaga Ruge Mutahaba

Muktasari:

Ni mmoja wa mameneja wa mwanamuziki Diamond Platnumz


Babu Tale ambaye ni mmoja wa mameneja wa mwanamuziki, Diamond Platnumz amefika katika viwanja vya Karimjee inapoendelea shughuli ya kumuaga aliyekuwa Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji, Ruge Mutahaba.

Uwepo wa Babu Tale na Harmonize katika viwanja hivyo umekuwa kivutio kutokana na uhasimu wa kibiashara uliopo baina ya Clouds Media Group na Wasafi Media.

Mbali na Babu Tale, kutoka Wasafi Media, Rommy Jones ambaye ni Dj na kaka wa Diamond Platnumz,  amekuwa miongoni mwa waombolezaji waliofika.

Rommy Jones pia ni mume wa mzazi mwenza wa Ruge Mutahaba anayefahamika kwa jina moja la Kay.

Mbali na Babu Tale na Rommy Jones, mamia ya waombolezaji wamejitokeza katika viwanja hivyo kumuaga Ruge ambaye pia ni mwanzilishi wa Semina za Fursa na tuzo za Malkia wa Nguvu.

Ruge Mutahaba alifariki Februari 26,2016 majira ya saa 1 usiku Afrika Kusini alipokuwa akipatiwa matibabu kwa miezi kadhaa.

Mwili huo utasafirishwa kwenda nyumbani kwao Bukoba katika Kijiji cha Kiziru kwa maziko ambayo yatafanyika keshokutwa.

Baadhi ya wasanii waliofika ni Hamisa Mobeto, Rich Mavoko, Abdu Kiba, Batuli, Shilole,Dogo Janja, Madee na wanamuziki wa THT.