Bunge la Tanzania laipitisha Bajeti ya Serikali ya mwaka 2019/2020

Wabunge wakiwa kwenye ukumbi wa bunge walipokuwa wakipiga kura kwa ajili ya kupitisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limepigia kura mapendekezo ya makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 na kupitisha kwa asilimia 78.2.

Dodoma. Bunge la Jamhuri ya Muungano la Tanzania limepitisha mapendekezo ya makadirio ya mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 ya Sh33.1 trilioni.

Akitoa matokeo ya shughuli ya upigaji kura ulivyokuwa, bungeni leo Jumanne Juni 25 2019, Katibu wa Bunge Stephen Kigaigai amesema jumla ya wabunge waliopiga kura ni  380.

Amesema  wabunge ambao hawakuwepo walikuwa ni 12 na hakuna mbunge ambaye hakuamua.

Kagaigai amesema wabunge waliosema hapana walikuwa ni  83 sawa na asilimia 21.8 ya wabunge waliopiga kura wakati wabunge 297  sawa na asilimia 78.2 walipiga kura za ndio.

Baada ya Kigaigai kutangaza matokeo hayo, Spika wa Bunge Job Ndugai ametangaza kuwa Bunge limekubali kupitisha makadirio hayo kwa asilimia 78.2.