Bibi wa miaka 77 akabwa koo, abakwa

Muktasari:

Bibi wa miaka 77 Jema Macheho (77) mkazi wa Bihawana jijini hapa amefariki dunia usiku wa kuamkia leo katika Hospitali ya Rufaa mkoani Dodoma baada ya kukabwa na kubakwa na kijana aliyetajwa kuwa na umri wa miaka 28 mkazi wa kijiji cha Chikoa.


Dodoma. Bibi kizee aliyejulikana kwa jina la Jema Macheho (77) mkazi wa Bihawana amefariki dunia baada ya kukabwa na kubakwa na kijana mmoja anayetajwa kuwa ni mkazi wa Chikoa mkoani hapa.

Akizungumza leo na waandishi wa habari Kamanda wa polisi mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema kwamba kikongwe huyo amefariki dunia majira ya saa tano usiku wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.

Muroto amesema tukio hilo limetokea Februari 11, mwaka huu majira ya saa mbili na nusu usiku wakati kikongwe huyo akiwa njiani huko Bihawana ndipo alipotokea kijana huyo aliyetajwa kuwa na umri wa miaka 28 ambaye alimvutia vichakani na kisha kumkaba shingoni na kumbaka.

“Watu wema walimfikisha hospitali na muda mfupi baadaye alifariki dunia kutokana na maumivu makali, mtuhumiwa amekamatwa na atafikishwa mahakamani kwa kosa la mauaji,” amesema Muroto.