Bilionea anayetafutwa kwa tuhuma dawa za kulevya afanyiwa upasuaji wa moyo

Mfanyabishara maarufu nchini Kenya, Ali Punjani

Muktasari:

Inaelezwa kuwa baada ya taarifa za kukamatwa kwake bilionea huyo alipata shambulio la moyo.

Mombasa, Kenya. Mfanyabishara maarufu nchini Kenya, Ali Punjani ambaye anatafutwa na polisi kwa tuhuma za usafirishaji wa dawa za kulevya amefanyiwa upasuaji wa moyo.

Taarifa kutoka katika familia yake zinasema kuwa bilionea huyo amelazwa katika Taasisi ya Moyo nchini India kutokaa na matatizo ya moyo.

Inaelezwa kuwa baada ya taarifa za kukamatwa kwake bilionea huyo alipata mshtuko na kusababisha ugonjwa wa moyo.

Msaidizi binafsi wa bilionea huyo, Kakawat Pankaj alisema kuwa kuwa Punjani alifanyiwa upasuaji wa moyo wiki iliyopita.

“Alipata shambulio la ugonjwa wa moyo na baada ya kufanyiwa uchunguzi katika Kituo cha magonjwa ya Moyo cha Mombasa walipata rufaa ya kwenda nchini India kwa matibabu zaidi,” alisema msaidizi huyo.  

Hata hivyo, polisi nchini Kenya imesisitiza kwamba itaendelea na taratibu za kesi hiyo ikiwamo kufanya upekuzi katika nyumba yake.

Msaidizi huyo alidhibitisha kupokea taarifa hiyo ya polisi na kusema kuwa mawakili wake watakuwa nyumbani kwake Nyali kesho ili kuruhusu maafisa wa polisi kufanya upekuzi huo.