VIDEO: Bunge la Tanzania lapata ripoti ya hesabu za CAG

Muktasari:

Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amesema taarifa ya ukaguzi wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) iliyofanywa na mkaguzi wa nje imekamilika na taarifa yake ameipeleka Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kwa ajili ya kuipitia.

Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amesema taarifa ya ukaguzi wa Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imekamilika huku akisema ‘katika ukaguzi hakuna anayejikagua mwenyewe.’

Akitoa taarifa hiyo leo Alhamisi Mei 16, 2019, bungeni, Spika Ndugai amesema kwa mujibu wa sheria ya ukaguzi wa umma, hesabu za ofisi ya CAG hupitiwa na Bunge kwa kuielekeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kufanya kazi hiyo.

“Hesabu za ofisi ya CAG zinapaswa kukaguliwa angalau mara moja kwa mwaka na Bunge kupitia kamati ya kudumu ya PAC huwa inajukumu la kuteua mkaguzi wa ofisi hiyo.”

“Kwa maneno rahisi, Bunge ndiyo tuna tafuta mkaguzi wa nje ambaye anakagua ofisi hiyo,” amesema Spika Ndugai.

Kiongozi huyo wa Bunge amesema tayari mkaguzi wa nje alipatikana na kukamilisha ukaguzi wake na taarifa yake imekamilika, “Nimeipokea, nimeshaipitia na taratibu zinanitaka niipeleke taarifa hiyo kwa PAC ili kuipitia na kuichambua.

“Baada ya kukamilisha watawasilisha taarifa kwangu, katika masuala ya ukaguzi hakuna anayebaki, hakuna anayejikagua mwenyewe,” ameongeza Spika Ndugai.