VIDEO: Bunge la Tanzania lamsamehe Masele

Muktasari:

Bunge la Tanzania limeridhia kumpuuza mbunge wa Shinyanga Mjini (CCM), Stephen Masele ambaye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ilimkuta na hatia ya kugonganisha mihimili na utovu wa nidhamu

Dodoma. Bunge la Tanzania limeridhia kumpuuza mbunge wa Shinyanga Mjini (CCM), Stephen Masele ambaye Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ilimkuta na hatia ya kugonganisha mihimili na utovu wa nidhamu.

Kamati hiyo ilipendekeza Masele ambaye pia ni makamu wa rais wa Bunge la Afrika (PAP) kusimamishwa kuhudhuria mikutano mitatu ya Bunge la Tanzania.

Ndugai ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Mei 23, 2019 bungeni jijini Dodoma baada ya kamati hiyo kuwasilisha taarifa yake hiyo.

Kabla ya wabunge kuanza kuchangia maoni ya kamati hiyo, Ndugai alihitimisha jambo hilo kwa kutaka Bunge kumpuuza Masele.

Mbali na kutaka kupuuzwa, Ndugai amesema amepokea ujumbe wa Masele kwamba anataka kuomba radhi.

Masele aliposimama alitoa tuhuma mbalimbali akidai Ndugai

amewasiliana na Rais wa  PAP ili amng’oe nafasi yake ya makamu wa Rais na ubunge wa Bunge hilo. Masele pia ameikataa taarifa ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge iliyomkuta na hatia.

Masele alihojiwa na kamati hiyo Jumatatu Mei 20, 2019 akituhumiwa na Ndugai kwamba amekuwa utovu wa nidhamu pamoja na kutoa maneno ya kugonganisha mihimili.

Ndugai alilieleza Bunge Mei 16, 2019 kwamba kutokana na utovu huo wa nidhamu amesimamisha uwakilishi wa Masele PAP ambako mkutano wa Bunge hilo ulikuwa ukiendelea nchini Afrika Kusini na kuagiza mbunge huyo kurejea nchini.

Alisema mara baada ya kurejea nchini, Masele atahojiwa na kamati hiyo pamoja na kamati ya maadili ya wabunge wa CCM.