CCM Dodoma wataka Makamba, Kinana washughulikiwe

Muktasari:

Halmashauri Kuu ya CCM mkoani Dodoma, imesema kitendo cha kuandika waraka na kulalamikia jina la mtu ni kinyume na utaratibu wa chama, hivyo wahusika washughulikiwe.

Dodoma. Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dodoma kimetaka makatibu wakuu wastaafu, Abdulahman Kinana na Yusuf Makamba washtakiwe kwa utovu wa nidhamu.

Akisoma tamko la Halmashauri ya CCM Mkoa, Katibu wa Siasa na Uenezi Hanry Msunga amesema mambo yaliyofanywa na wastaafu hao ni kinyume na taratibu za Chama.

Msunga amesema haiwezekani chama kikongwe kikahusishwa na mtu aliyemtaja kwa jina la Musiba, hivyo wanaamini yaliyofanywa na wastaafu hao ni ukiukwaji wa maadili.

“Lazima Chama kichukue hatua zaidi, jambo hilo ni kinyume kabisa na maadili, hawa wazee hawakustahili kufanya walichokifanya,” amesema Msunga huku akishangiliwa.

Awali, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Dodoma, Godwin Mkanwa alisema kazi zinazofanywa na Rais, John Magufuli zinapaswa kuungwa mkono na si kubezwa na mtu yeyote.

Mkanwa amesema chama hicho kinapongeza juhudi na kazi nzuri za kiongozi huyo na wao Dodoma ambako ni ngome ya CCM, wataendelea kuziunga mkono kazi zozote za kiongozi huyo mkuu wa nchi.