Christian Bella atinga Ikulu na Hamisa Mobetto

Muktasari:

Mkali wa masauti. Ndivyo anavyojiita mwanamuziki, Christian Bella ambaye jana Alhamis Juni 13, 2019 aliambatana na mwanamitindo Hamisa Mobetto Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kupewa mwaliko na Rais John Magufuli

Dar es Salaam. Mkali wa masauti. Ndivyo anavyojiita mwanamuziki, Christian Bella ambaye jana Alhamis Juni 13, 2019 aliambatana na mwanamitindo Hamisa Mobetto Ikulu jijini Dar es Salaam baada ya kupewa mwaliko na Rais John Magufuli.

Bella alipewa mwaliko huo kwa ajili ya kusherehesha hafla ambayo Rais Magufuli alimuandalia  Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Felix Tshisekedi aliyeadhimisha miaka 57 ya kuzaliwa.

Mwanamuziki huyo aliambatana na mwanamitindo huyo kutokana na kumshirikisha katika wimbo wake mpya wa Boss alioutoa siku za hivi karibuni. Tukio la kuimba pamoja na Mobetto katika jukwaa ni la kwanza tangu alipotoa wimbo huo.

Bella amemshukuru kiongozi mkuu huyo wa nchi kwa kumpa mwaliko, akibainisha kuwa ni mara yake ya pili kufika Ikulu kwa ajili ya kutumbuiza, kusisitiza kuwa wimbo huo umeanza na baraka, anatarajia kuwa utafanya vyema zaidi.

Miaka mitatu iliyopita mwanamuziki huyo alialikwa Ikulu na Rais Magufuli baada ya rais mstaafu wa DRC, Joseph Kabila kutembelea nchini.