Dakika 75 za majibizano ya risasi polisi, watuhumiwa wa ujambazi

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Jonathan Shanna akionesha silaha iliyokamatwa wilayani Ngorongoro baada majambazi wawili kuuawa wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha leo.Picha na Filbert Rweyemamu

Muktasari:

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Jonathan Shana amesimulia jinsi polisi walivyojibizana kwa risasi na watuhumiwa wawili wa ujambazi kwa muda wa dakika 75. Amesema wawili wamefariki dunia na mmoja ametoroka.


Arusha. Jeshi la Polisi mkoani Arusha limewaua watu wawili wanaotuhumiwa kuwa ujambazi katika tukio la majibizano ya risasi lililodumu kwa dakika 75 katika  eneo la mlima Digodigo wilayani Ngorongoro.

Watuhumiwa hao waliokutwa na bunduki ya kivita aina ya AK 47, walikuwa wakisakwa na polisi kwa tuhuma za unyang’anyi wa kutumia silaha na kuteka magari ya watalii na kuwapora.

Akizungumza leo Jumatano Juni 12, 2019 kamanda wa polisi Mkoa wa Arusha, Jonathan Shana amesema tukio hilo limetokea juzi, baada ya upekuzi mmoja alikutwa na bunduki hiyo ikiwa na risasi 20.

Amewataja waliofariki dunia kuwa ni, Kulima Albart (33) mkazi wa kijiji cha Muholo na Hashimu Nginodya (28) mkazi wa Digodigo.

“Walikuwa wakifanya uhalifu maeneo mbalimbali ya Loliondo, walirushiana risasi na polisi kwa dakika 75 ila mtuhumiwa mmoja ametoroka,” amesema Shana.