Dengue yaendelea kutikisa Dar

Muktasari:

Licha ya hatua mbalimbali kuendelea kuchukuliwa na mkoa wa Dar es Salaam kukabiliana na Dengue, idadi ya wagonjwa imeendelea kuongezeka

Dar es Salaam. Idadi ya wagonjwa wa homa ya Dengue katika mkoa wa Dar es Salama imeendelea kuongezeka na sasa wamefikia 1,809 kutoka 1,200 wiki iliyopita.

Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa amesema takwimu za hadi jana zinaonyesha kuna jumla ya wagonjwa 1,901 ambao wameshaugua ugonjwa huo, huku kati yao 1,809 wakiwa katika mkoa wa Dar es Salaam.

Ongezeko hilo ni wagonjwa 674 sawa na wastani wa wagonjwa 75 kwa siku huku kata ya Ilala ikitajwa kuongoza kwa kuwa na wagonjwa 235.

Profesa Kambi amesema idadi hiyo inaonyesha kuwa bado kuna kazi kubwa ya kufanya kuhakikisha watu wanapata elimu na kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo.

Amesema hatua mbalimbali zimeendelea kuchukuliwa ikiwamo kutoa elimu, kuhamasisha usafi wa mazingira kuondoa mazalia ya mbu pamoja na kuhimiza wagonjwa kuwahi hospitali.

Kwa upande wa matibabu, Profesa Kambi amesema Serikali imehakikisha hospitali na vituo vyake vya afya vinakuwa na uwezo wa kupima ugonjwa huo huku vitendanishi vingine vikiendelea kuagizwa kutoka nje ya nchi.

“Tumeagiza ‘taste kits’ 3000 ambazo zina uwezo wa kupima watu 30,000. Kati ya hivi 200 ziko tayari na tutazisambaza kwenye hospitali za Dar es Salaam na nyinginezo  zitakuja,” amesema.

Profesa Kambi ametumia fursa hiyo kuwasihi Watanzania kuacha taarifa za mitandaoni kuhusu uwapo wa tiba ya ugonjwa huo na badala yake kusikiliza maelekezo yanayotolewa na Serikali.