Diamond, Zari wapigana vijembe kisa kuchepuka

Muktasari:

  • Diamond amemtuhumu Zari kuchepuka na mwanamuziki wa Nigeria, Peter ambaye ni mmoja wa mapacha wanaounda kundi la P Square

Mwanamuziki Diamond na aliyekuwa mpenzi wake, Zari wamerushiana tuhuma kupitia radio, televisheni na mitandao ya kijamii .

Diamond ndiye aliyeanza wakati akitambulisha wimbo wake mpya wa  ‘The One’ kupitia Wasafi Radio na televisheni ambapo alieleza sababu za kuachana na mwanamke huyo mwaka mmoja uliopita kuwa alichepuka na mwanamuziki wa Nigeria, Peter ambaye ni mmoja wa pacha wanaounda kundi la P Square.

Alieleza kuwa mbali na Peter, pia mwanadada huyo alichepuka na mwalimu wa mazoezi na ndiyo sababu iliyomsukuma kumfanyia visa mwanamke huyo mpaka akatangaza kumuacha.

“Mimi sijawahi kuachwa na mwanamke, akinifanyia mambo mabaya nampiga matukio mpaka mwenyewe anajiondoa, hivyo ndivyo ilivyokuwa pia katika uhusiano wangu na Zari,” alijigamba.

Naye Zari ambaye siku za hivi karibuni amekuwa akimnadi mpenzi wake mpya kupitia mtandao wa Instagram alijibu mapigo akisema Diamond ameamua kutumia jina lake kwa kuwa muziki wake haukiki.

“Pale ambapo muziki wako unakuwa hauna nguvu tena unabaki kutumia jina la Zari ili usikike, mimi sijawahi kuchepuka wakati nipo naye na ninajiapiza kama nimewahi kufanya hivyo basi lolote liwatokee watoto wangu,” aliandika Zari kwa mafumbo na kuendelea:

“Sasa kama mtu amewahi kuikana damu yake kuna uongo gani mwingine anaweza kuacha kusema? Ni vyema kukiri makosa yako na kuyatumia kukua, bado unayo nafasi,” alihitimisha.