Dk Mwinyi: Mishahara ya wanajeshi huongezwa kuanzia ngazi ya juu hadi ya chini

Muktasari:

Serikali imetoa ufafanuzi kuhusu mishahara na posho za Jeshi kwamba zinaongezwa kuanzia ngazi ya juu.

Dodoma. Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussen Mwinyi amesema mishahara ya wanajeshi huongezwa kuanzia ngazi ya juu na kushuka chini.

Akijibu hoja za wabunge wakati wa kuhitimisha hotuba yake leo Alhamisi Mei 16,2019, Mwinyi amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa unaofanywa na vikosi vya jeshi.

Amesema kwa sasa Serikali inafanya mapitio ya kuona jinsi ya kuwasaidia wanajeshi kuboresha maisha yao kusudi waweze kufanya kazi zao kwa uhuru.

Akijibu hoja za kambi ya upinzani, Waziri Mwinyi ametaja suala la sare za jeshi ambalo lilizua mjadala akisema hakuna mwanajeshi anayepatiwa nguo pana au ndogo, bali wote hupimwa kupitia kampuni halali zinazoshindanishwa tenda na kushinda.

Amesema nguo pekee ambazo huwa zimeshonwa moja kwa moja ni kombati za jeshi ambazo nazo wanapewa nafasi ya kuchagua kulingana na umbile la mtu.

Katika hatua nyingine, Waziri Mwinyi amewaomba wabunge kuacha kuzungumzia kazi zinazofanywa na vikosi vya jeshi katika masuala ya kisiasa kufanya hivyo watakuwa wanawavunja moyo wanajeshi.

Kuhusu upandishwaji vyeo, amesema kazi hiyo hufanywa kwa uadilifu lakini akatahadharisha kuwa, siyo kila anayekwenda kozi lazima apandishwe cheo kwa kuwa kuna vitu vingi vya kuzingatiwa.