Dk Tulia: Sh1 bilioni kumaliza mafuriko Mbeya

Muktasari:

  • Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson amesema Sh1 bilioni zimetengwa kwa ajili ya kumaliza changamoto ya mafuriko jijini Mbeya.

Dar es Salaam. Naibu Spika wa Bunge, Dk Tulia Ackson amesema mkoa wa Mbeya umeanza mpango maalumu wa kudhibiti mafuriko na unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 11 huku ukigharimu zaidi ya Sh1 bilioni.

Kuanzishwa kwa mpango huo kunatokana na athari za mafuriko kwa kaya zaidi ya 100 katika kata ya Nzovwe jijini hapo.

Ameyasema hayo leo katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Ruanda, Nzovwe jijini Mbeya leo Aprili 26, 2019.

“Fedha hizi zitatuondolea maafa haya kwa sababu kila mwaka tunakuwa ni waathirika kwa sababu eneo hili lina mvua nyingi,” amesema Dk Tulia.

Alitumia nafasi hiyo pia kumuomba Rais kuwachangia katika kuendeleza ujenzi wa kituo cha afya cha Itezi ikiwa ni baada ya wananchi kuonyesha nia ya kuanza kujenga kituo hicho.

“Tunashukuru pia kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya katika kata ya Nzovwe kwa sababu umetoa kipaumbele kwa afya ya wananchi ili waweze kufanya kazi vizuri lakini tunashukuru pia kwa ajili ya ukarabati wa shule ya wasichana Loleza na shule ya Iyunga,” amesema Dk Tulia.

“Tunaomba utusaidie tuanze kufanya biashara zetu katika eneo la Mbeya kiwanja cha ndege na hata kama kuingia mikataba sisi tuko tayari kufanya hivyo,” amesema.