Ebola yatua Uganda, WHO yathibitisha

Muktasari:

Ugonjwa wa ebola umezidi kuwa tishio DRC na hivi sasa umeingia nchi jirani ya Uganda baada ya mtoto kubainika kuwa na kuthibitishwa na shirika la afya duniani (WHO).


Kampala. Mtoto wa miaka mitano nchini Uganda amebainika kuwa na ebola, Shirika la Afya Duniani (WHO) limethibitisha.

Hiki ni kisa cha kwanza kuthibitishwa katika nchi hiyo wakati kukishuhudiwa mlipuko wa ugonjwa huo katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) .

Imeelezwa kuwa mtoto huyo wa kiume alisafiri na familia yake na kuvuka mpaka kutoka DRC siku ya Jumapili.

Baada ya hapo alipelekwa katika hospitali moja Uganda kutokana na kuonyesha dalili ya ugojwa huo hasa kutapika damu.

Uthibitisho kwamba amekuwa na ebola ulitolewa na Taasisi ya Kupambana na Virusi Uganda (UVRI) jana Jumanne na kutangazwa rasmi.

 Kwa mujibu wa Wizara ya Afya nchini Uganda na WHO, wametuma kikosi maalumu kutambua wengine walio katika hatari ya kupata ugonjwa huo.

Waziri wa Afya Uganda, Jane Ruth Aceng amewaambia waandishi wa habari kwamba familia ya mtoto huyo inaangaliwam kutokana na kuonyesha kuwa na dalili za za ebola.

Wahudumu 4, 700 Uganda wamepewa chanjo dhidi ya ugonjwa huo, taarifa hiyo ya pamoja ya shirika la afya duniani na wizara ya afya nchini imeendelea kueleza.