Fid Q kunadi magari yake kumjibu Babu Tale

Muktasari:

Hata hivyo, kumiliki magari pia sio kipimo cha mafanikio

 


Sakata la majibizano kati ya Meneja wa WCB, Babu Tale na msanii wa muziki wa kizazi kipya  Farid Kibanda ’Fid Q’, limeingia katika sura mpya baada ya msanii huyo kudai kuwa ataanika magari yake anayoyamiliki leo.

Majibizano kati ya wawili hayo yalipamba moto jana katika mtandao wa Instagram, ambapo Babu Tale alimtuhumu Fid Q kwamba pamoja na kuwa msanii  wa siku nyingi hata gari hana na maisha anayoishi ni ya kulelewa na mwanamke.

MCL Digital leo Novemba 21, ilimtafuta Fid Q kujua ukweli wa tuhuma hizo ambaye alieleza ilitokana na tangazo lake la kunogesha tamasha la Fiesta ambapo yeye ni mmoja wa wasanii watakaotumbuiza siku hiyo.

Hata hivyo amesema tuhuma zote zilizotolewa dhidi yake  hakuna lenye ukweli hata moja na kama ni gari anayo magari huku akiahidi kuyaanika leo, ili kutoupa uongo nafasi.

Wakati kuhusu kulelewa, msanii huyo amesema:“Labda aniambie ule ubwabwa mtamu aliokuta akala siku aliyekuja kwangu ulimnogea na kuona ununuaji wa mchele uliwezeshwa na shemeji yake.

“Isitoshe Wabongo wanapaswa kuelewa kwamba kuishi na Mzungu au kuwa na mahusiano naye haimaanishi kwamba unalelewa kwani na wao wana maisha kama yetu tu na pia ishu ya kumiliki gari sio sababu ya kuonekana kuwa una mafanikio na kwangu sio kitu nilichokipa kipaumbele,’ amesema msanii huyo wa kibao cha Mwanza.