Gwajima: Haturudi nyuma

Muktasari:

  • Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima amesema kanisa hilo litasonga mbele katika utoaji huduma, huku akibainisha kuwa mtu aliyechimba shimo atatumbukia mwenyewe na mtego alioutega umpate mwenyewe

Dar es Salaam.  Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima amesema kanisa hilo litasonga mbele katika utoaji huduma, huku akibainisha kuwa mtu aliyechimba shimo atatumbukia mwenyewe na mtego alioutega umpate mwenyewe.

Ametoa kauli hiyo leo Jumapili Mei 12 katika kanisa lake lililopo Ubungo jijini Dar es Salaam, ambapo alisema awali alikuwa akimtilia shaka Askofu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF),  Zachary Kakobe lakini kutokana na mahubiri aliyoyatoa leo katika kanisa lake, hana shaka naye tena.

Awali, katika mahubiri yake Kakobe alizungumza picha za video zinazosambaa mitandaoni zikimuonyesha mtu anayefanana na Gwajima akiwa faragha na mwanamke ambaye bado hajafahamika na kueleza kuwa zimesambazwa baada ya viongozi wa kiroho kuwa wamoja.

“Mnong'oneze jirani yako mwambie zimeingia kokoto unatoka unga yaani hii ni mashine ya kukoboa kusaga,” amesema Gwajima na kushangiliwa na mamia ya waumini wa kanisa lake.