Halmashauri zakwama kupata fedha za miradi ya Kimkakati

Muktasari:

Ujuzi mdogo wa kuandika miradi ya maendeleo katika halmashauri wakwamisha halmashauri kupata fedha za miradi ya kimkakati nchini.

Arusha. Halmashauri nyingi nchini, zimekwama kupata fedha za miradi ya kimkakati, kutokana na kushindwa kuandika vizuri miradi ya maendeleo yenye tija .

 

Hadi kufikia sasa ni halmashauri 29 kati ya halmashauri  185 tu ndio miradi yake 37  ya kimkakati imekubaliwa na kupatiwa fedha  kiasi cha sh 268 bilioni.

 

Akifungua mafunzo ya jinsi ya kuandika miradi ya kimkakati, katika halmashauri, ambayo yaliandaliwa na benki ya maendeleo (TIB) na Bodi ya mikopo ya serikali za Mitaa, jana Jumatatu Machi 11, 2019 Katibu tawala mkoa wa Arusha, Richard Kwitega alisema watendaji wa halmashauri ambao watashindwa kuandika miradi baada ya mafunzo watakuwa hawatoshi katika nafasi zao.

 

"Ni imani ya serikali kuwa mafunzo ambayo mtapata hapa kwa siku mbili, yatawasaidia kuweza kuandika miradi kwa kuzingatia vigezo na kama ikishindikana basi mtaonekana hamtoshi katika nafasi zenu," alisema

 

Alisema mafunzo hayo ambayo yanashirikisha watendaji 120 wa halmashauri za mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Manyara ni fursa nyingine kwa watendaji kujifunza kuandika miradi bora yenye tija na sio kuandika mawazo ya miradi.

 

Kwitega alisema halmashauri nyingi nchini, zimekwama kupata fedha za mikopo na kutoka serikalini kutokana na kushindwa kutimiza vigezo vya kupata fedha za miradi ya kimkakati ambayo inahitajika katekelezwa.

 

Mkurugenzi wa Mipango, mikakati na mawasiliano wa benki ya Maendeleo(TIB), Patrick Mongella alisema miradi mingi ambayo imeombewa fedha katika benki hiyo, imekwama kutokana na kutoandikwa vizuri na mingine kuonekana kama wazo na sio mradi.

 

"TIB tumekuwa tukitenga fedha kwa ajili ya kutekelezwa miradi ya kimkakati lakini ni halmashauri nyingi zinashindwa kupata fedha kutokana na kutokuwa na ujuzi wa kuandika miradi kulingana na vigezo" alisema

 

Akizungumza katika mafunzo hayo, Mjumbe wa timu ya uchambuzi wa miradi ya kimkakati kutoka Ofisi ya Rais Tawala za mkoa na serikali za mitaa(TAMISEMI),Iddi Mshiri alisema kuna vigezo 14 zimewekwa ili mradi uwezo kukubaliwa na kupewa fedha.

 

Alisema serikali hadi sasa ni halmashauri 28 tu ndizo zimeweza kuandika vyema miradi na kukubaliwa jambo kiasi cha Sh268 bilioni zitatolewa na serikali.

 

Kaimu katibu wa bodi ya mikopo kwa serikali za mitaa, Yeremiah Mahinya alizitaka halmashauri nchini, kutumia vizuri fursa ya mikopo na fedha kutoka serikali, kwa kuandika miradi ambayo inakopesheka na yenye tija katika jamii.

 

Mafunzo hayo yanashirikisha maafisa 120 wa halmashauri za kanda ya kaskazini na Shinyanga ikiwa ni mfululizo wa mafunzo yanayotolewa na benki ya maendeleo TIB na  bodi ya mikopo ya serikali za mitaa ,