Ilemela, Arusha, Musoma kuchota 8.1 bilioni

Muktasari:

Kuanzia kesho Ijumaa Mei 17, 2019 hadi Jumatatu Mei 20,2019, Serikali itaanza kulipa fidia maeneo ya wananchi wa mkoani Arusha, Ilemela na Musoma na Sh 8.1 bilioni zitalipwa.


Dodoma. Kuanzia kesho Ijumaa Mei 17, 2019 hadi Jumatatu ya Mei 20,2019, Serikali imesema italipa fidia ya Sh8.1 bilioni katika maeneomatatu ambayo iliyatwaa kwa matumizi ya jeshi.

Naibu Waziri wa Fedha , Dk Ashatu Kijaji amesema leo Alhamisi Mei 16,2019 bungeni kwamba serikali imetenga fedha hizo jana.

Dk Kijaji ameyataja maeneo yanayokwenda kulipwa niya Ilemela ambayo imetengewa Sh3.5 bilioni, Arusha Sh3.5 bilioni na eneo la Musoma zilikotengwa Sh1.1 bilioni.

Amesema wakati fedha hizo zikitengwa jana, tayari Serikali imeshatoa Sh50 milioni kwa mthamini mkuu wa serikali kwa ajili ya kufanya uthamini eneo la Kakonko mkoani Kigoma.

Hoja ya Kijaji ilikuja pale wabunge walipoibana serikali kuhusu fidia kwa maeneo mbalimbali iliyoyachukua kwa ajili ya matumizi ya majeshi.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri, Serikali inapitia maeneo mengi kukamilisha uthamini ili waweze kulipa fidia na kuondoa migogoro baina ya wananchi na Jeshi.