Kinywaji cha kuongeza nguvu chenye viagra chapigwa marufuku

Muktasari:

Uchunguzi umebaini kuwa kinywaji hicho kimechanganywa na chembechembe za dawa hiyo inayotumika kusaidia matatizo ya nguvu za kiume

 

Serikali nchini Zambia zimepiga marufuku kinywaji cha kuongeza nguvu baada ya uchunguzi wa maabara kuonyesha kina kiambato cha dawa ya Viagra inayorejesha nguvu za kiume.

Kinywaji hicho, SX Energy Natural Power, kinachotengenezwa na Revin Zambia, huuzwa hata nje ya nchi, ikiwemo Uganda, ambako mteja mmoja alilalamika hivi karibuni kuwa alipata tatizo la kusimamisha uume kwa muda mrefu na kutoka jasho jingi.

Katika taarifa yake juzi, Serikali katika jiji la Ndola ambako kiwanda hicho kipo, iliamuru "bidhaa ya kinywaji cha nguvu kubwa za asilia ya SX iondolewe (madukani)".

Msemaji wa jiji la Ndola, Tilyenji Mwanza alisema katika taarifa hiyo kuwa matokeo kutoka Zimbabwe na Afrika Kusini yanafanana na vipimo vilivyofanywa Zambia ambavyo vinaonyesha "kuwepo kwa kemikali ya Sildenafil Citrate".

Mwezi Desemba mwaka jana, mamlaka inayosimamia dawa ilisema kuwa kinywaji hicho kilichanganywa Sildenafil Citrate - dawa inayotumika kutibu tatizo la nguvu za kiume na kimetolewa chini ya chapa ya Viagra.

Maofisa wa Revin Zambia hawakuweza kupatikana kuzungumzia suala hilo.