Lady Gaga aufuta wimbo alioimba na R Kelly, aomba radhi

mwanamuziki R Kelly 

Muktasari:

Auondoa katika mitandao yao akiwaunga mkono mabinti waliodai kunyanyaswa kingono na R Kelly

 


Majanga yameendelea kumuandama mwanamuziki R Kelly baada ya kurushwa kwa jarida la Surviving R Kelly takribani wiki tatu zilizopita akituhumiwa kuwanyanyasa kingono mabinti wadogo.

Safari hii mwanamuziki Lady Gaga ameuondoa katika mitandao yote wimbo Do What You Want alioimba na mwanamuziki huyo miaka mitano iliyopita huku akiomba radhi.

Kupitia mtandao wa Twitter Lady Gaga alitangaza uamuzi wake wa kuuondoa wimbo huo huku akisema anafanya hivyo kuwaunga mkono mabinti waliopitia kadhia hiyo.

“Ninawaunga mkono mabinti hao kwa asilimia 1,000, malalamiko yao yanapaswa kusikilizwa na kuungwa mkono. Alichofanya R Kelly ni kitendo cha kinyama ambacho hakuna lugha yoyote duniani inaweza kukitetea,” aliandika Lady Gaga.

Lady Gaga amesema akiwa mmoja wa wanawake waliowahi kunyanyaswa kingono, anaumia kila anaposikia walichofanyiwa mabinti hao hivyo hawezi kunyamaza.

Wimbo Do What You Want aliurekodi mwaka 2013 akimshirikisha R Kelly mwenye umri wa miaka 52.