Magufuli: Mikutano ya siasa haijazuiwa

Rais John Magufuli

Muktasari:

 

  • Rais John Magufuli amesema hakuna kiongozi aliyezuiliwa kufanya mikutano ndani ya jimbo lake bali wanapaswa kuzingatia taratibu za kupata vibali

Dar es Salaam. Rais John Magufuli amesema hakuna kiongozi aliyezuiwa kufanya mkutano katika jimbo lake bali kilichozuiwa ni kwenda kufanya mikutano katika majimbo ya wengine tena kwa fujo.

Amesema kufanya hivyo ni sawa na askofu kutoka katika kanisa lake na kwenda kuwatukana watu msikitini jambo ambalo linaweza kuvuruga amani.

“Kama ninyi mnavyoheshimiana na sisi tunataka vyama vyetu vya siasa hata kama vipo 50 viheshimiane,” amesema.

“Nataka kuwahakikishia viongozi wa dini hakuna mtu aliyezuiliwa kufanya mkutano halali mahali alipo na bahati nzuri kwa mujibu wa sheria wanaotoa vibali ni polisi ukienda utapewa.”

“Wamefanya Dar es Salaam hapa sitaki kueleza yaliyotokea maana yapo mahakamani, wamefanya chaguzi zao ni mikutano, kwa hiyo nataka kukuhakikishia baba Mchungaji Lymo (Amani) hakuna mtu aliyezuiliwa kufanya mikutano,” amesema Rais Magufuli.

Amesema anataka vyama viige mifano ya viongozi wa dini wanavyoheshimiana na kusaidiana kwa sababu moja ya jambo analozingatia ni amani.

“Kama ni mbunge wa Ubungo afanye mkutano muda wote hakuna anayemzuia kwa sababu yeye ndiyo anawaongoza afanye mheshimiwa Kubenea (Saed) kwa sababu mimi naamini hiyo ndiyo demokrasia nzuri inayotakiwa.’’

Amesema ndiyo maana hivi sasa huwezi kumsikia Hillary Clinton akizunguka kufanya mikutano sehemu mbalimbali bali ni Donald Trump pekee kwa sababu ndiyo muda wake na atapimwa katika kipindi kilichopangwa.