Magufuli afanya uteuzi Bodi ya Airtel Tanzania, TTCL

Rais wa Tanzania, John Magufuli 

Muktasari:

Rais Magufuli amemteua Dk Omari Nundu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Airtel Tanzania ikiwa ni utekelezaji wa makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na kampuni ya Bharti Airtel International.


Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amemteua Dk Omari Nundu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania ikiwa ni utekelezaji wa makubaliano yaliyofikiwa kati ya Serikali na kampuni hiyo ya Bharti Airtel International.

Katika makubaliano hayo, Mwenyekiti wa Bodi ya Airtel Tanzania pamoja na ofisa mkuu wa ufundi wanapaswa kuteuliwa na Serikali.

Taarifa iliyotolewa leo Jumatano Juni 12, 2019 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa imesema pia Rais Magufuli amemteua Mohammed Mtonga kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) akichukua nafasi ya Dk Omari Nundu.

Pamoja na Dk Nundu, Serikali pia imemteua Dk Prosper Mafole kuwa ofisa mkuu wa ufundi kwa mujibu wa makubaliano hayo.

“Wajumbe wengine watakaoiwakilisha Serikali katika Bodi ya Airtel Tanzania ni John Sausi na Lekinyi Mollel. Uteuzi huu unaanza leo tarehe 12 Juni, 2019,”  amesema Msigwa.