Magufuli ampigia Ndugai kampeni ‘kiaina’

Muktasari:

Rais wa Tanzania, John Magufuli amempigia kampeni ‘kiaina’ mbunge wa Kongwa (CCM), Job Ndugai akiwataka waliokuwa washindani wake katika mchakato wa kura ya maoni ya chama hicho mwaka 2015, kumuacha aendelee kuwa mbunge kwa maelezo kuwa anatosha

 


Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amempigia kampeni ‘kiaina’ mbunge wa Kongwa (CCM), Job Ndugai akiwataka waliokuwa washindani wake katika mchakato wa kura ya maoni ya chama hicho mwaka 2015, kumuacha aendelee kuwa mbunge kwa maelezo kuwa anatosha.

Magufuli  ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Julai 18, 2019 alipokuwa akizungumza na wananchi wa Kongwa jijini Dodoma.

Ametumia fursa hiyo pia kuwashukuru wananchi wa Kongwa kumchagua kwa kura nyingi alipowania urais mwaka 2015.

 “Ndugai ni mtoto wenu, ninafahamu wakati wa kampeni kuna wengine walitaka ubunge na nilipofika hapa niliwaambia kazi sio ubunge tu.”

“Na kweli wale wote waliogombea na Ndugai niliwateua nafasi mbalimbali, wengine wakawa wakurugenzi na wengine wakuu wa wilaya,” amesema Magufuli.

Ameongeza, “Nitawashangaa sana kama mwaka 2020 watakuja kugombea hapa na wakija wajue ukuu wa wilaya, ukurugenzi na hawatauona tena. Ninalisema hili kwa dhati labda wajitokeze wengine,” amesema

Huku akimsifia Spika huyo wa Bunge, Magufuli amesisitiza, “Lakini pia nazungumza kwa dhati kwa sababu huyu anatosha, mimi Kongwa nina historia nayo inawezekana msijue kwani  dereva ambaye ameniendesha wakati nikiwa waziri wa ardhi, waziri wa vitoweo na sasa ni zaidi ya miaka 23 anatoka hapa.”