Majaji waahirisha kwa muda kesi ya viongozi wa upinzani Tanzania

Muktasari:

  • Viongozi wa vyama vya upinzani nchini Tanzania wakiongozwa na Freeman Mbowe wamefungua kesi katika Mahakama ya Afrika Mashariki iliyopo jijini Arusha wakipinga sheria mpya ya vyama vya siasa  nchini humo. Kesi hiyo inasikilizwa leo Jumatano katika mahakama hiyo

Arusha. Majaji wa Mahakama ya Afrika ya Mashariki wameahirisha kesi ya kupinga sheria mpya ya vyama vya siasa kwa muda ili kufanya majadiliano kama  waendelee kusikiliza kesi upande mmoja wa walalamikaji ama kuishirikisha Serikali ya Tanzania.

Majaji wanaosikiliza shauri hilo leo Jumatano Juni 19, 2019 ni  Monica Mugenyi kutoka Uganda, Dk Faustine Ntezilyayo (Rwanda) Dk Charles Nyawelo (Sudani kusini) Charles Nyachai (Kenya) na Fakihi Jundu (Tanzania) .

Mawakili wa vyama vya upinzani wameomba Mahakama hiyo kutoa uamuzi wa dharura kusitisha sheria hiyo na baadaye kuendelea na kesi ya msingi kwani tayari michakato ya uchaguzi imeanza.

Katika kesi ambayo imehudhuriwa na idadi kubwa ya viongozi wa upinzani wa Tanzania na wawakilishi wa mashirika yasiyo ya kiserikali kusikiliza uamuzi unaotarajiwa kutolewa leo Jumatano.