Majaliwa atoa angalizo matumizi reli Tanga-Kilimanjaro

Muktasari:

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amezitaka kamati za ulinzi Mikoa ya Kilimanjaro na Tanga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya reli ya Tanga-Kilimanjaro kuepuka ajali


Moshi. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amezitaka kamati za ulinzi Mikoa ya Kilimanjaro na Tanga kutoa elimu kwa wananchi kuhusu matumizi ya reli ya Tanga-Kilimanjaro kuepuka ajali.

Ametoa kauli hiyo leo Jumamosi Julai 20, 2019 katika uzinduzi wa treni ya mizigo itakayofanya safari zake kati ya Tanga na Kilimanjaro.

Amesema ni jukumu la viongozi kuwapa elimu wananchi kuhusu matumizi sahihi ya reli, “Kamati za ulinzi na usalama katika Mikoa ambayo reli inapita watoe elimu kwa wananchi kuepuka ajali kwa sababu sheria inasema mtu akikanyagwa na treni yeye ndio anakuwa ameigonga treni.”

Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi ya Shirika la Reli Tanzania (TRC), Profesa John Kondoro amesema lengo la kuifufua reli hiyo iliyotumika mara ya mwisho miaka 12 iliyopita ni kurahisisha usafirishaji wa mizigo.

“Serikali imetoa fedha za ukarabati wa mabehewa 200, kuna wadau wametusaidia kukarabati vichwa vya treni 40, tunaomba wadau wengine wajitokeze,” amesema.