Makonda: Hatutatumia nguvu kuondoa mifuko ya plastiki Dar
Muktasari:
- Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemhakikishia makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan kuwa nguvu haitatumika katika utekelezaji wa kuondoa matumizi ya mifuko ya plastiki kuanzia Juni Mosi, 2019.
Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amemhakikishia makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan kuwa nguvu haitatumika katika utekelezaji wa kuondoa matumizi ya mifuko ya plastiki kuanzia Juni Mosi, 2019.
Aprili 9, 2019 Serikali ilipiga marufuku matumizi ya mifuko hiyo na kubainisha kuwa haitakiwi kutumika kuanzia Juni Mosi, 2019.
Makonda ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Mei 27, 2019 katika kikao cha viongozi wa jijini Dar es Salaam kilichofanyika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Julius Nyerere.
"Tutakwenda kutekeleza maagizo yako vizuri, jambo zuri ni kwamba athari za mifuko hii zinajulikana.
Kampeni hii ni tofauti na ile ya kupambana na dawa za kulevya ambayo ilikuwa na ugumu wake.”
“Wakazi wa Dar es Salaam ni waelewa na wameshaanza kuchukua Makamu wa Rais hutopata shida ndani ya mkoa huu," amesema Makonda.
Mkuu huyo wa Mkoa amesema kesho kutakuwa na hafla ya kuonyesha mifuko mbadala ili kuhakikishia mifuko hiyo inapatikana.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), January Makamba, naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Mwita Waitara.
Wengine ni wakuu wa wilaya zote tano za jijini Dar es Salaam, wakurugenzi, mameya na maofisa waandamizi wa Mkoa wa Dar es Salaam.