Makonda aja na kongamano la kuwasaidia wajane

Mkuu wa mkoa was Dar es Salaam,Paul Makonda akionyesha mfano wa fomu watakayoijaza wajane watakaokwenda kwa ajili ya huduma ya msaada wa kisheria.

Muktasari:

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda awageukia wajane mkoa huo aandaa kongamano maalumu kwa ajili yao ilih kusikiliza kero zao ikiwemo suala la mirathi.

Dar es Salaam. Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ameandaa kongamano maalumu la wajane ili kusikiliza na kutatuta changamoto zao.

Akizungumza na wanahabari leo, Jumanne Aprili 2, 2019, Makonda amesema kwamba kongamano hilo litafanyika Alhamisi hii Aprili 4, 2019 katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.

Makonda amesema kina mama wajane wanakumbana na changamoto kuu mbili ambazo ni kutokuwa na wenzi baada ya kufariki dunia na changamoto ya pili ni kudhulumiwa haki zao na ndugu wa upande wa mume.

"Nawaomba wajane wote siku hiyo ili tuweze kuwasaidia na shughuli itaanza saa moja kamili asubuhi. Tutakuwa na wanasheria na wadau mbalimbali wakiwemo Tamwa (Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania)," amesema Makonda.

Ameongeza: "Nina imani kila atakayekuja ni mjane na si vinginevyo na kutakuwa na utaratibu ikiwemo fomu zitakazojazwa na wajane kuhusu taarifa zao."