VIDEO: Makonda awapa siku tano wakurugenzi Ilala, Kinondoni

Muktasari:

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ametoa siku tano kwa wakurugenzi wa manispaa za Ilala na Kinondoni kuhakikisha ujenzi wa miradi iliyotengewa fedha ya machinjio ya Vingunguti na Ufukwe wa Coco inaanza.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es  Salaam, Paul Makonda ametoa siku tano kwa wakurugenzi wa manispaa za Ilala na Kinondoni kuhakikisha ujenzi wa miradi iliyotengewa fedha imeanza.

Kauli hiyo ameitoa leo Ijumaa Machi 22, 2019 alipokutana na wakuu wa wilaya na watendaji kujadili miradi ambayo haijafikia malengo.

Amesema kwa mkoa wa Dar es Salaam ziko fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi ikiwemo machinjio ya Vingunguti na uendelezwaji wa Ufukwe wa Coco.

"Natoa siku tatu kwa mkurugenzi wa Ilala  awe amesaini mkataba wa machinjio ya Vingunguti na mkurugenzi wa Kinondoni awe amesaini mkataba wa uendelezwaji wa Ufukwe wa Coco na ndani ya siku tano miradi hiyo iwe imeanza," amesema Makonda.

Amesema fedha hizo ni za miradi ya kimkakati ndani ya mkoa ambazo zilishatolewa na Rais John Magufuli na ziko kwenye akaunti lakini miradi hiyo imekuwa haitekelezwi .

"Fedha zilishatolewa na Rais Magufuli kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wa mkoa wa Dar es salaam cha kushangaza hakuna mradi ulioanza," amesema.

Ameongeza kwa watendaji wote watakaotekeleza miradi chini ya kiwango watawajibika kwa kuwa huo ni ubadhirifu wa fedha za uma.