VIDEO: Mama aliyejifungia watoto wanne anena

Muktasari:

  • Binti wa miaka 24, mkazi wa Magomeni Chemchem Jijini Dar es Salaam aliyejifungua watoto wanne, anaomba msaada kutoka kwa wadau mbalimbali kumsaidia mahitaji muhimu ya watoto kutokana na hali yake ya maisha kuwa ngumu.

Dar es Salaam. Watoto ni baraka. Lakini unapopata watoto zaidi ya wawili ‘pacha’ changamoto huanza kuonekana katika malezi na namna ya kuwatunza kama ilivyotokea kwa Radhia Solomon (24) na mumewe Fami Suleiman (28).

Watoto hao wa kike wawili Faudhia na Fardhia pamoja na wa kiume wawili Suleiman na Aiman ni pacha ambao kila mmoja alikuwa na mfuko wake wa uzazi.

Tangu Radhia ajifungue pacha hao wanne Januari 8 mwaka huu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), ametaja changamoto kadhaa zinazomfanya ashindwe kuwatunza vema wanawe kutokana na gharama za huduma.

Akizungumza na Mwananchi nyumbani kwake Magomeni Chemchem jijini Dar es Salaam, Radhia ambaye tangu ajifungue siku 63 zimepita, amesema kwa kipindi chote hicho watoto wamekuwa wakitumia maziwa ya Sh40,000 kila siku.

“Nilipojifungua sikuwa na afya nzuri na damu yangu ilishuka na kufika 3, nilishindwa kunyonyesha watoto hivyo walianzishiwa maziwa ya SMA ambayo ni Sh40,000, wao wanakunywa kwa siku kopo moja ambalo haliwezi kumaliza siku ya pili,” amesema Radhia.

Amesema mumewe ambaye kwa sasa hana kazi amejitahidi kuhudumia kwa kipindi hicho chote lakini kwa sasa hali ya uchumi imekuwa mbaya zaidi kiasi cha kuhitaji msaada.

Unaweza kutuma mchango wako kupitia namba 0682604202 Radhia Solomon.

Kupata undani wa habari hii soma nakala ya Mwananchi kesho Jumanne Machi 12,2019