Man United yamziba mdomo Mourinho

Kocha wa Manchester United Jose Mourinho 

Muktasari:

Kocha wa Manchester United Jose Mourinho amesema hana  haraka kufanya uamuzi wa kujiunga na klabu mpya, baada ya kutimuliwa Old Trafford

London, England. Baada ya kulipwa fungu kubwa baada ya kuvunjiwa mkataba, Jose Mourinho ameamua kupumzika kabla ya kurejea kibaruani.

Man United imemlipa kocha huyo stahiki zake  zote zinazofikia Pauni15 milioni baada ya kuvunja mkataba.

Chanzo cha karibu na kocha huyo kilidai hana mpango kujiunga na klabu mpya kwasasa.

 “Hana anachodai baada ya kumalizana na Manchester ingawa ana fursa ya kujiunga na klabu nyingine, lakini hana haraka,” kilisema chanzo hicho.

Chanzo hicho kilisema Mourinho (55), yuko katika hali njema baada ya kukwaruzana na uongozi wa Man United.

Mourinho yuko huru kujiunga na klabu nyingine akitaka baada ya kumalizana na Man United ingawa hana haraka kufanya uamuzi.

Kocha huyo alifukuzwa Desemba 18, baada ya kufanya kazi kwa miaka miwili na nusu bila mafanikio akichukua nafasi ya Louis Van Gaaal.

Mourinho amewahi kuzinoa kwa nyakati tofauti FC Porto, Inter Milan, Real Madrid, Chelsea kabla ya kujiunga na Man United.