Mbowe, Matiko kutema nyongo

Muktasari:

  • Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mbunge wa Tarime, Esther Matiko watazungumza na waandishi habari jijini Dar es Salaam, ikiwa ni siku chache baada ya kutoka rumande walikokaa kwa siku 104

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na Mweka Hazina wa Baraza la wanawake la chama hicho (Bawacha), Esther Matiko watazungumza na waandishi wa habari kesho Ijumaa Machi 15, 2019 jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo unakuja baada ya viongozi hao ambao pia ni wabunge kusota rumande kwa siku 104 baada ya kufutiwa dhamana Novemba 23, 2018.

Hata hivyo, Machi 7, 2019 wawili hao walishinda rufaa yao waliyoikata Mahakama Kuu ya Tanzania kupinga kufutiwa dhamana na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi Machi 14, 2019 na mkuu wa idara habari na mawasiliano wa Chadema, Tumaini Makene imesema viongozi hao watazungumza na waandishi wa habari katika Hoteli ya Golden Tulip katikati ya Jiji.

Tangu walipoachiliwa huru, si Mbowe ambaye ni kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani Bungeni au Matiko waliozungumza kile walichopitia au kukishuhudia wakiwa gereza la Segerea.