VIDEO: Mbowe alivyomzungumzia Profesa Lipumba

Muktasari:

Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe amempa salaam Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akisema muda utaeleza anachokifanya sasa.

Dar es salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amempelekea salaam Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba akisema muda utasema kwa anayofanya.

Mbowe ameyasema hayo leo Ijumaa Machi 15, 2019 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

Salamu za Mbowe zinakuja wakati CUF upande wa Profesa Lipumba ukikamilisha mkutano mkuu uliomrejesha madarakani kama mwenyekiti, huku upande wa Maalim Seif Sharif Hamad ukisisitiza kuwepo kwa zuio la Mahakama.

Amesema licha ya kutofautiana na Profesa Lipumba bado anamheshimu, “ila muda ndio utasema kama analofanya ni sahihi au si sahihi. Nawaombea tu wamalizane salama," alisema.

Mbowe amesema mivutano unaoendelea kwenye chama hicho ni ya kutengeneza ili kukandamiza demokrasia.

"Inasababishwa na dhamira ya kudhoofisha vyama vya upinzani na kudhoofisha misingi ya haki katika taifa," amesema Mbowe.

Akizungumzia upande wa Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif, Mbowe amesema haki aliyodai ilidhulumiwa katika uchaguzi wa 2015 itarejea siku moja.

"Nimwombee Maalim Seif na timu yake watambue kwamba mapito (yana mwisho)," alisema.