Mbunge Chadema adai naibu Waziri wa Viwanda anaomba rushwa

Muktasari:

  • Mbunge wa Ndanda (Chadema), Cecil Mwambe ameibua tuhuma bungeni dhidi ya naibu Waziri wa Viwanda, Stella Manyanya akidai anakwamisha juhudi za Serikali kwa kuwaomba rushwa wawekezaji.

Dodoma. Mbunge wa Ndanda (Chadema), Cecil Mwambe ameibua tuhuma bungeni dhidi ya naibu Waziri wa Viwanda, Stella Manyanya akidai anakwamisha juhudi za Serikali kwa kuwaomba rushwa wawekezaji.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Mei 17, 2019 katika mjadala wa bajeti ya Wizara ya Kilimo mwaka 2019/2020, akibainisha kuwa Manyanya anapaswa kuwa miongoni mwa wanaotakiwa kuwajibishwa.

Huku akieleza tamaa yake ya kuwa miongoni mwa mawaziri wa Viwanda ili amsaidie kazi Rais John Magufuli, Mwambe aliibua tuhuma hizo muda mfupi baada ya Manyanya kulieleza Bunge kuwa baadhi ya wabunge wa vyama vya upinzani wanachunguzwa kwa kuomba rushwa kampuni mbalimbali.

Ameitaka Serikali kuwawajibisha mawaziri waliohusika na mkataba mbovu wa ununuzi wa korosho kati ya Tanzania na kampuni ya Indo Power Solution ya Kenya.

Mbunge huyo amesema maeneo mbalimbali ambayo kamati ya Bunge ya Viwanda na Biashara imetembelea, wamekuta tuhuma za Manyanya kuomba rushwa na kusababisha wawekezaji kuogopa.