Mbunge aituhumu mahakama, Mwanasheria Mkuu wa Tanzania ajibu

AG, Profesa Adelardus Kilangi

Muktasari:

  • Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Amina Mollel ameituhumu mahakama kwa kutokutoa haki dhidi ya baba aliyedaiwa kumbaka mtoto wake, hata hivyo, Ofisi Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) nchini Tanzania imesema inalifuatilia suala hilo.

Dodoma. Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) nchini Tanzania inafuatilia sakata la mtoto wa miaka 11 anayedaiwa kubakwa na baba yake mzazi, Aristerico Silayo ambaye licha ya kutiwa hatiani, aliachiwa guru.

Kauli hiyo imetolewa bungeni leo Alhamisi Juni 27, 2019 na AG, Profesa Adelardus Kilangi akisema kesi hiyo ilikuwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha.

Profesa Kilangi ametoa kauli hiyo wakati akijibu hoja za wabunge katika mjadala wa muswada sheria ya marekebisho ya sheria mbalimbali namba 3 wa mwaka 2019 kufuatia mwongozo wa Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Amina Mollel, ambaye alihoji kuhusu uamuzi wa Mahakama kumwachia huru baba aliyembaka mwanae mkoani Arusha.

Katika hoja yake mbunge hiyo amesema licha ya  mtuhumiwa huyo kupatikana na hatia, mtoto huyo amekosa haki katika mahakama ya Arusha baada ya mtuhumiwa kuachiwa huru.

“Naibu Spika, nina masikitiko makubwa nikiwa kama mama, ninasimama kwa ajili ya kusimamia haki ya mtoto ambaye amekosa haki katika mahakama ya Arusha,” amesema Mollel.

Amesema mtoto huyo kwa muda mrefu alikuwa akibakwa na baba yake mzazi kwa kuingiliwa mbele na nyuma hivyo kuharibika kwa kiasi kikubwa.