Mchakato wa kampuni 100 bora waanza

Mkurugenzi wa kampuni ya Mwananch Communication LTD,Francis Nanai(katikati) akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tuzo za makampuni 100 bora za kati uliofanyika jijini Dar es Salaam jana. Picha na Said Khamis

Muktasari:

  • Mchakato wa kutafuta kampuni bora 100 bora za kiwango cha kati awamu ya tisa umezinduliwa leo Alhamisi Julai 11, 2019 huku Benki ya CRDB ikitangazwa kama mdhamini mkuu wa mashindano hayo mwaka 2019.

Dar es Salaam. Mchakato wa kutafuta kampuni bora 100 bora za kiwango cha kati awamu ya tisa umezinduliwa leo Alhamisi Julai 11, 2019 huku Benki ya CRDB ikitangazwa kama mdhamini mkuu wa mashindano hayo mwaka 2019.

Uzinduzi huo umefanyika leo ambapo waandaaji ambao ni Kampuni ya Hesabu ya KPMG na Kampuni ya Mwananchi Communication’s Ltd (MCL), wameungana wadhamani wengine wa shindano hilo.

Wadhamini wengine ni mfuko wa kuendeleza huduma za kifedha nchini (FSDT), kampuni ya Azam Media Group na hoteli ya Serena.

Akizungumza katika uzinduzi huo mkurugenzi wa KPMG Tanzania, Ketan Shah amesema, “ Ili kufanikiwa na kustawi katika biashara ni muhimu kupata faida na kuwa na maendeleo. Natoa wito kwa kampuni za kati kujitokeza kushiriki katika shindano hili litawasaidia kukuza biashara zao na masoko.”

Mkurugenzi Mtendaji wa MCL,  Francis Nanai amewashukuru wadhamini wa shindano hilo akisisitiza kuwa ana imani watapata thamani halisi ya matarajio yao katika kuwaunga mkono na kutoa wito kwa kampuni nyingi kujitokeza.

"Kumekuwa na mafanikio makubwa katika mashindano haya, tunafurahi kuwa na CRDB kama mdhamini mkuu hii inaashiria wabia wa uchumi wanathamini mchango unaotokana na mashindano haya muhimu kwa maendeleo ya Taifa," amesema Nanai.

Nanai amesema watu wengi wamekuwa na kiu ya kuona mashindano hayo yanafanyika mikoani na ameahidi hilo litafanyika endapo hali ya kifedha itaruhusu.

Amesema vigezo vya kushiriki ni kampuni kuwa na mapato ya mwaka kati ya Sh1 bilioni hadi Sh20 bilioni na hesabu zake ziwe zimekaguliwa.

Amebainisha kuwa taratibu za kushiriki na taarifa nyingine zinapatikana kupitia matangazo katika magazeti yanayochapishwa na kampuni ya MCL ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti,  mitandao ya kijamii, televisheni na njia nyinginezo

Mkurugenzi wa CRDB,  Abdulmajid Nsekela amesema shindano hilo linaendana na mpango wa benki hiyo wa kukuza biashara na masoko sanjari na kuongeza idadi ya mabilionea nchini.

Mkurugenzi wa operesheni wa FSDT, Irene Mlola amesema, “Tutafurahi kuwashirikisha namna bora ya kufanya biashara zao kukua zaidi kwa kuangalia ni changamoto gani hasa wanakutana nazo na kuzitafutia ufumbuzi.”